MSANII wa muziki wa hip hop nchini, Young Killer, anatarajia kuachia kibao chake kipya kinachokwenda kwa jina la ‘Mrs Super Star’ hivi karibuni.
Msanii huyo kwa sasa anatamba na kibao chake cha ‘Dear Gambe’, ambacho ameimba na Belle 9.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Young Killer alisema yupo katika hatua za mwisho za uandaaji wa kibao hicho, ambacho anaamini kitafanya vizuri kutokana na ubora wa mashairi yaliyomo ndani yake.
“Naamini kazi hii itafanya vizuri kutokana na mashairi ya wimbo huo, naomba wapenzi wa kazi zangu wakae mkao wa kula kwa ajili ya kuipokea,” alisema.
Young Killer alisema kwa upande wa video ya ngoma hiyo, wataonekana baadhi ya wasanii ‘Mastaa’ wa kike ambao wanafanya vizuri katika tasnia ya filamu.
Aliwataja wasanii watakaoonekana katika video ya kazi hiyo kuwa ni Elizabeth Michael ‘Lulu’, Irene Uwoya ‘Oprah’, Jacqueline Wolper, Wema Sepetu na mwanamitindo, Jokate Mwogelo.






