Watu zaidi ya mia moja wanahofiwa
kufa baada ya kuangukiwa na kifusi katika machimbo ya dhahabu ya
wachimbaji wadogo wadogo ya kalole yaliyoko katika kata ya msalala
wilayani kahama mkoani shinyanga na inasemekana wachimbaji hao walivamia
mgodi baada ya muda wa kazi hali iliyosababisha mashimo manane ya mgodi
huo kutobozana na hatimaye nguzo kuvunjika na kisha kifusi kuwaangukia.
ITV ilifika katika eneo hilo na kukuta zoezi la kutambua maiti
linaendelea na wakaguzi wakiendelea na zoezi la kukagua mashimo
yaliyokuwa wazi huku baadhi ya wachimbaji walionusurika katika tukio
hilo wakiulalamikia ulinzi wa machimbo hayo kuwa ndio chanzo cha tukio
hilo kwakuwa tukio lilitokea mapema saa kumi na mbili baada ya saa za
kazi lakini inashangaza taarifa kupatikana saa sita za usiku na wamedai
kuwa idadi ya watu waliofukiwa na kifusi ni zaidi ya mia na hamsini
lakini serikali imeridhika na idadi ya watu kumi na tisa ambao
wameshaopolewa hadi wakati huu.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa jeshi la polisi
mkoa wa shinyanga Justus Kamugisha amesema watu hao walivamia mgodi
baada ya muda wa kazi kuisha na kulingana na wingi wao mgodi ulielemewa
na kusababisha nguzo kuvunjika hali iliyosababisha kifusi kuwaangukia
lakini kwa jitihada za jeshi la polisi tayari wameshaopolewa watu kumi
na tisa na kumi na mbili kati yao wameshatambuliwa na tayari
wameshachukuliwa na ndugu zao tayari kwa maziko.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya kahama Bw. Benson Mwampesya
amesema kwakuwa imeonekana idadi ya vijana walioangukiwa na kifusi ni
wengi zaidi ya hao walioopolewa serikali imeamua kuomba wataalam na
mitambo ya kuchimba eneo hilo kutoka katika mgodi wa bulyanhulu
unaomilikiwa na kampuni ya acacia ili kuharakisha zoezi la kuhakiki kuwa
hakuna maiti zingine zilizonaswa katika mashimo ya mgodi huo.